1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya Kenya kukatia rufaa uamuzi kuhusu BBI

14 Mei 2021

Mwanasheria mkuu nchini Kenya ameanza rasmi hatua ya kukata rufaa kufuatia uamuzi wa mahakama kuu kusitisha mchakato wa maridhiano BBI, uliolenga kuibadili katiba kupitia kura ya maoni.  

https://p.dw.com/p/3tNxQ

Mwanasheria mkuu nchini Kenya ameanza rasmi hatua ya kukata rufaa kufuatia uamuzi wa mahakama kuu kusitisha mchakato wa maridhiano BBI, uliolenga kuibadili katiba kupitia kura ya maoni.  

Naibu wa rais William Ruto amefurahishwa na uamuzi wa mahakama, ambao amesema unawatendea haki raia wa kawaida. Mswada wa BBI uliungwa mkono kwa kishindo na wabunge na maseneta ulipowasilishwa mbele yao.

Mwanasheria Mkuu Paul Kihara Kariuki ameanza rasmi harakati za kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa majaji watano waliosema kuwa mchakato wa BBI unakiuka sheria na katiba.

Wakili mkuu wa serikali ya Kenya Ken Ogeto aliweka bayana kuwa mwanasheria mkuu anaruhusiwa kisheria kukata rufaa.

Kwa sasa tayari mwanasheria mkuu ameshawasilisha malalamiko rasmi kusitisha kwa muda uamuzi wa mahakama kuanza kufanya kazi. Kilichowakirihi wanaounga mkono mchakato wa maridhiano wa BBI ni kwamba mahakama iliamua kuwa mswada huo unakiuka sheria na katiba.

Rais Kenyatta alaumiwa kwa kushindwa kuheshimu katiba 

Kenia Symbolbild Wahlen und Social Media
Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya Picha: AFP/T. Karumba

Kwa mtazamo wa mwanasheria mkuu Paul Kihara, mswada huo ulipata ridhaa ya umma kwani ulipata saini milioni 3 kuendelea kufanyiwa kazi.

Bunge la taifa na baraza la senate kadhalika liliuidhinisha mswada wa BBI ulipowasilishwa mbele yao.Kwa mantiki hii ipo haja ya kufafanua ukiukaji wa sheria kama ilivyotamka mahakama kuu.

Jopo la majaji watano ambao ni Teresia Matheka, Joel Ngugi, George Odunga, Jairus Ngaah na Chacha Mwita lilimshutumu Rais Uhuru Kenyatta kwa kushindwa kuiheshimu, kuitetea na kuilinda katiba ya Kenya jambo linalozitia doa sifa za kuwa kiongozi wa taifa.

Kimsingi hoja ya kutaka kuifanyia katiba mageuzi ilipaswa kuwasilishwa na raia wa kawaida na wala sio kusukumwa na rais.

Mahakama pia ilisema kuwa kamati ya usimamizi wa mchakato wa BBI sio halali na kwamba harakati zote za tume ya kitaifa ya uchaguzi IEBC mintarafu mswada huo zimefutiliwa mbali.
 

Ruto na wafuasi wake washusha pumzi 


Kwa upande wa pili,naibu wa Rais William Ruto alielezea furaha yake baada ya mahakama kuifutilia mbali shughuli ya kuibadili katiba.Kupitia ukurasa wake wa Twitter Naibu wa Rais William Ruto aliandika kuwa amefurahi sana na kwamba Mungu aliye mbinguni anaipenda Kenya mno.

Kenia Symbolbild Wahlen und Social Media
Picha: AFP/T. Karumba

William Ruto alikuwa mstari wa mbele kuunga mkono mchakato utakaowapa nafasi wakenya kuhoji na kubadili vipengee vinavyowatatiza katika katiba na wala sio hati yote kwa jumla.

Kadhalika aliipinga hoja ya kuwaruhusu wanasiasa kuwateua makamishna wa tume ya uchaguzi ya kitaifa IEBC.

Ifahamike kuwa Jaji Joel Ngungi na George Odunga waliokuwa wanachama wa jopo lililoutupilia mchakato wa BBI ni baadhi ya majaji 41 ambao rais Uhuru Kenyatta bado anasubiriwa kuwapa ridhaa kujiunga na makahakama ya rufaa.