1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump na Biden: Wagombea 2 wazee wawania wapigakura vijana

Carla Bleiker | Iddi Ssessanga
2 Machi 2024

Joe Biden na Donald Trump, ambao huenda wakakabiliana katika uchaguzi ujao wa rais wa Marekani baadae, wote ni wazee. Lakini umri wao una jukumu gani katika kinyang'anyiro hicho, na wanaweza kuwavutia wapiga kura vijana?

https://p.dw.com/p/4cvRN
Picha ya pamoja Joe Biden na Donald Trump
Wapigakura nchini Marekani huenda wakalaazimika tena kuchagua kati ya wazee wawili, Joe Biden na Donald Trump katika uchaguzi wa Novemba 2024.

Uchaguzi wa mchujo chamani bado unaendelea, lakini ukiondoa mfadhaiko mkubwa, kinyang'anyiro cha urais wa Marekani 2024 kitakuwa marudio ya 2020: Joe Biden dhidi ya Donald Trump. Hiyo ina maana kwamba siku ya uchaguzi, Novemba 5, 2024, wapiga kura wanaweza kuchagua kati ya mzee Trump mwenye umri wa miaka 78 Trump na Biden mwenye umri wa miaka 81. Iwapo hivyo ndivyo itakavyokuwa, mshindi atakaeapishwa Januari 20, 2025, atakuwa ndiye mtu mzee zaidi kuwahi kuapishwa kuwa rais wa Marekani.

Umri wa wastani wa marais wa awali wa Marekani wakati wa kuapishwa ulikuwa 55, kulingana na Kituo cha Utafiti cha Pew. Iwe Biden au Trump atakaeshinda, rais hatakuwa na umri wa miaka 50 wakati huu - atakuwa katika au ataingia miaka ya 80 akiwa madarakani. Wakati huo huo, umri wa wastani wa idadi ya watu wa Marekani ni miaka 38.9, kulingana na Ofisi ya Sensa ya Marekani.

Marekani San Francisco 2024 | Rais Biden akiwasili kwenye mkutano wa kampeni
Ikiwa atamaliza muhula wa pili kama rais, Joe Biden atakuwa na umri wa miaka 86 wakati anaondoka Ikulu mnamo Januari 2029.Picha: Manuel Balce Ceneta/AP Photo/picture alliance

Ndiyo maana haishangazi, umri umekuwa jambo muhimu kabla ya uchaguzi wa mwaka huu.

"Kuna wasiwasi kuhusu umri. Wasiwasi huo ni halali kabisa," Larry Sabato, mkurugenzi wa Kituo cha Siasa cha Chuo Kikuu cha Virginia, aliiambia DW. "Sidhani kwamba watu wanapaswa kuhukumiwa tu kwa umri wao. Wakati huo huo, ni dhahiri kwamba unapokuwa mkubwa, una nafasi kubwa zaidi ya kuwa na matatizo makubwa ya afya au kukutana na muumba wako mapema kabla hujapanga."

Soma pia: Kwanini suala la umri wa rais Joe Biden ni mjadal

Rais Biden amechanganya mara kwa mara majina ya viongozi wa dunia na watu mashuhuri. Hivi karibuni, alipoulizwa kuhusu mzozo wa Mashariki ya Kati wakati wa mkutano wa waandishi wa habari, alimtaja Abdel Fattah el-Sissi kimakosa kuwa rais wa Mexico - el-Sissi ni rais wa Misri, na Mexico iko Amerika Kaskazini, sio Mashariki ya Kati. Biden pia anaonekana kutokuwa na nguvu za kimwili wakati anapoonekana kuliko wakati alipofanya kampeni za urais mara ya mwisho.

"Sio umri wenyewe unaowapa [watu] wasiwasi," mwandishi makala mliberali na mwandishi vitabu Ezra Klein alisema kwenye podikasti yake "The Ezra Klein Show." "Ni hisia ambazo Biden anatoa kuhusu umri. Za kwenda polepole. Za udhaifu."

Biden azidi kupongezwa kwa ushindi licha ya Trump kukataa kukubali kushindwa

'Umri wa Biden ni tatizo'

Trump anapambana na maswala ya kiafya, pia, pamoja na kuwa mzito. Na amekuwa na aina zile zile za kuteleza ambazo Biden amekuwa nazo. Kwa mfano, alichanganya China na Korea Kaskazini alipodai katika hotuba yake mwezi Novemba kwamba "Kim Jong Un anaongoza watu bilioni 1.4." Pia alichanganya balozi wake wa zamani wa Umoja wa Mataifa, Nikki Haley, na Nancy Pelosi, ambaye alikuwa spika wa Bunge katika nusu ya pili ya muhula wake pekee wa urais.

Hata hivyo, wapiga kura vijana waliozungumza na DW walisema wana wasiwasi kuhusu umri wa Biden hasa.

Soma pia: Je, ni wagombea wepi wanaowania uteuzi wa vyama Marekani?

"Sina imani kwa asilimia 100 iwapo [mgombea] yeyote kati yao anaweza kufanya kazi kikamilifu, lakini nadhani Trump ana nafasi nzuri zaidi kutokana na yeye kuonekana kuwa imara zaidi,'" alisema Zack, 26, kutoka Midwest, ambaye hakupendelea kutaja jina lake la mwisho kwa sababu za faragha. "Wakati mwingine ninapomwangalia Biden, nahisi kama hajui kinachoendelea hata kidogo."

Makamu wa Rais wa Marekani Kamala Harris
Licha ya umri wake mdogo, Kamala Harris hajaweza kuamsha shauku miongoni mwa wapiga kura wa chama cha Democratic.Picha: Misper Apawu/AP/picture alliance

Wasiwasi sawa na huo unaendelea miongoni mwa vijana wanaopinga sera za Trump na, kutokana na chaguo kati ya Trump na Biden, wangependelea aliye madarakani abakie rais.

"Sikubaliani na siasa nyingi za Trump, na, kwa hivyo, umri wa Biden ni shida kwa sababu, kwa kulinganisha na Trump, anaonekana dhaifu kidogo," alisema James W., 29, ambaye anaishi katika Jiji la New York na pia akachagua kutotataka kutaja jina lake la mwisho.

"Kwa bahati mbaya, nadhani Trump angeweza kufanya kazi yake vizuri zaidi kuliko Biden," alisema Emma Lengel, mwenye umri wa miaka 23 mkazi wa Washington DC. "Lakini hakuna anaefaa kati yao, na Trump kufanya kazi yake vizuri haina mantiki kwa Marekani."

Wagombea vijana hawawezi kupenya

Vyama vya Republican na Democrats vilikuwa na wagombea wadogo katika kinyang'anyiro hicho kwa wakati mmoja, lakini hakuna aliyeweza kuwatikisa vigogo wa vyamani. Kwa upande wa Republican, Niki Haley, 52, na Gavana wa Florida Ron DeSantis, 45, walizingatiwa kama wagombea wenye matumaini kufikia hadi 2023. Lakini wakati Haley akisalia kwenye kinyang'anyiro hicho, hakuna Mrepublican ambaye ameweza kupinga udhibiti wa Trump kwenye chama.

Soma pia: Trump arudi kortini mkesha wa ushindi unaotarajiwa New Hampshire

Kwa upande wa chama cha Democrats, itakuwa jambo lisilo la kawaida sana kwa mtu yeyote kumpinga Biden, rais aliyeko madarakani, kwa uteuzi wa chama. Hapo awali, wagombea kadhaa vijana walishindana dhidi yake kwa nafasi ya juu wakati wa mchujo wa 2020, akiwemo waziri wa sasa wa uchukuzi Pete Buttigieg, ambaye sasa ana umri wa miaka 42, na Makamu wa Rais Kamala Harris, 59.

Marekani | Ron DeSantis
Gavana wa Florida Rod DeSantis alijitoa kwenye kinyang'anyiro cha uteuzi wa chama cha Repiblican na kutangaza kumuunga mkono mzee Trump.Picha: Anna Moneymaker/AFP/Getty Images

Wakati Harris alipotangazwa kwa mara ya kwanza kama mgombea mwenza wa Biden, waangalizi wengine walikisia kwamba umri wake utamzuia kuchaguliwa tena na anaweza kuwa anayefuata kwenye nafasi hiyo. Lakini Harris ameshindwa kuboresha wasifu wake kwa miaka minne iliyopita, na pia hajachochea shauku ya kutosha miongoni mwa wapiga kura wa Kidemokrasia kwa chama kumpigia kamari kuhusu Biden.

Choshwa na 'wanasiasa wa zamani, wasiozingatia uhalisia'

Uzee haumweki mgombea moja kwa moja katika hasara au kumzuia kuwasiliana na wapiga kura vijana. Seneta wa Vermont Bernie Sanders, ambaye, akiwa na umri wa miaka 82, ni maarufu kwa wanafunzi wa chuo kikuu na wahitimu wa hivi karibuni, anathibitisha hilo.

Mkazi wa Washington Lengel pia alisema uzee sio sababu ambayo kwake ingeondoa moja kwa moja wagombea. Lakini ukosefu wa hatua juu ya maswala ambayo yalikuwa muhimu kwa Wamarekani vijana ni sababu.

"Wanahitaji kushughulikia wasiwasi wetu," alisema. "Nimechoka sana na wanasiasa hawa wa zamani, wasio na mawasiliano wanaojaribu kupata alama za brownie kwa kutuunga mkono wakati, kwa kiwango cha sheria, hawafanyi chochote."

Soma pia:Trump aanza vyema safari yake ya kuwania urais Marekani 

Rachel Lee, 24, ambaye pia anaishi Washington, alisema anahisi kama "(Trump na Biden) hawaelewi kikamilifu matatizo ya vijana siku hizi."

Marekani| Seneta Bernie Sanders
Katika umri wa miaka 82, Seneta wa Marekani Bernie Sanders ameweza kuamiliana vyema na wapiga kura vijanaPicha: Kena Betancur/AFP/Getty Images

Trump, Biden 'uzee kutosha kuwa mababu zangu'

Marais wazee wameweza kuamiliana na wapiga kura vijana hapo awali. "[Rais Ronald] Reagan aliondoka madarakani akiwa na umri wa karibu miaka 78," mtaalamu wa siasa Sabato alisema. "Unajua kiwango cha umaarufu wake kilionyesha nini? Vijana walikuwa wakimuunga mkono sana. Walikuwa wakimuona kama babu."

Katika kesi ya Reagan, hiyo ilionekana kuwa faida. Lakini wapiga kura vijana wa leo wana mashaka zaidi kuhusuBiden na Trump.

"Nadhani wanawakilisha baadhi ya maoni yangu, lakini wana umri wa kutosha kuwa babu na babu yangu," Zack alisema. "Ni wangapi kati yenu ambao wana maoni sawa na mababu zenu?"

James pia anahisi kukumbushwa wazee wake na Trump na Biden - na sio kwa njia nzuri.

"Kila ninapowatazama wakizungumza, ninahisi kama nawatazama babu na bibi yangu wakishughulishwa na jambo fulani," alisema. "Lazima nitikise kichwa na kusema 'hakika' kwa sababu ninahisi kama hawataelewa tatizo lolote."

Kinachokuja, mwishowe, ni kukosa mawasiliano kati ya wapiga kura vijana na wanasiasa ambao ni umri wa babu na bibi zao.

"Ili kuwafikia vyema zaidi vijana [wapiga kura], vyama vinahitaji kufanyia kazi na kuboresha masuala yanayoathiri zaidi kizazi chetu," alisema Lee.